Mambo Mawili (2) Ya Msingi Ya Kuzingatia Katika Msamaha Wa Kweli


Msamaha ni kuondoa uchungu ulioumbika ndani ya moyo wako kwa hiari yako mwenyewe na kwa makusudi yako mwenyewe. Kusamehe ni kumfutia mtu deni. Kwa hiyo kama hujasamehe unadaiwa deni hivyo yakupasa usamehe kwa faida yako mwenyewe. Kusamehe ni amri na ni agizo la Mungu. Unaposamehe unakua unarudisha uhusiano uliopotea kati ya mkosa na mkosewa. Unaposamehe unakua unatoa uchungu ulioumbika moyoni mwa mtu na kuwa huru kimwili, kiakili na kiroho. Kutosamehe ni kubeba mzigo wa hiari ndani ya moyo wako. Samehe ili uweze kusamehewa.

Sio mara yako ya kwanza kusikia dhana ya kusamehe saba mara sabini mpaka leo hii. Huenda ulikuwa hujui nini maana ya kusamehe saba mara sabini. Kusamehe saba mara sabini maana yake kila siku hapa duniani unatakiwa kusamehe. Kwani ukizidisha saba mara sabini utapata mia nne na tisini hivyo basi, ndani ya mwaka kuna siku 365 inakupasa kusamehe hata zaidi ya mara moja ndio maana ya saba mara sabini ambayo unapata siku 490. Kwa hiyo msamaha hauna mwisho kila siku wewe ni kusamehe tu. Samehe kwa faida yako mwenyewe. Samehe hata kwa kulia machozi lia kabisa uondoe uchungu ulioumbika ndani ya moyo badala ya kubeba mzigo wa kutosamehe.

Leo tutajifunza kitu kipya kabisa katika somo la msamaha. Karibu ndugu msomaji, na yafuatayo ni mambo mawili (2) ya msingi ya kuzingatia katika msamaha wa kweli.

*1. Kitu Cha Kwanza Ni Kuchunguza Kiini Cha Kosa/Tatizo. Kabla hujafanya msamaha wowote chunguza kwanza kiini cha kosa au tatizo ni nini? Usifanye msamaha kabla hujajua kiini cha kosa au tatizo. Katika maisha yako, huenda umepitia mapito mengi na kujeruhiwa sana lakini huna budi kusamehe. Usiposamehe maana yake unaendelea kubaki na uchungu ndani ya moyo wako. Unachunguza kiini cha kosa ni nini? Pengine mtu anakuchukia tu bila sababu yoyote, anakuwa na wivu tu, ukifanya kitu kizuri hapongezi, mwingine tamaa inamuongoza nk.

Mfano halisi, kuna watu wanapatwa na uchungu kwa wengine kufanikiwa, mwenzako akipandishwa cheo kazini unakasirika unanuna kabisa sasa ukichunguza kiini cha kosa na kugundua mtu anakuchukia kwa sababu ya wewe kupandishwa cheo, kuonywa, kuambiwa ukweli na nk. ‘’ignore’’ puuzia na samehe kwa faida yako ukiona huna kosa na msalimie hata kama haitiki. Na ukichunguza ukiona huna kosa basi wewe msamehe na ukiona wewe ndio unakosa jishushe na rudi katika msamaha wa kweli.

Inapotokea makazini upo na wenzako halafu wanakuambia kuna dili la pesa hivyo unatakiwa ushiriki katika rushwa na wewe hutaki sasa na wewe ukakataa kushiriki je wale wafanyakazi wenzako watakua na mahusiano mazuri tena na wewe? Hapana hawawezi kuwa na mahusiano mazuri na wewe tena watakuita majina ya bandia kama vile mwacheni huyo mlokole na maneno mengi yanayohusiana na hayo.

Sasa katika mfano huu ukichunguza kiini cha kosa au tatizo utagundua nani ni mkosa au mkosewa kama ukiona huna kosa baada ya kuchunguza kiini cha kosa katika jambo hilo puuza na endelea na maisha yako na kama wewe ndio mkosa omba msamaha. Hivyo basi, mpaka sasa ndugu msomaji, umeshapata picha nzima ya kuchunguza kiini cha kosa. Kwa hiyo, kabla hujafanya msamaha chunguza kwanza kiini cha kosa ili kujua nani ni mkosa/msababishi wa kosa na nani ni mkosewa.

*2. Kitu cha pili ni kutambua kosa. Ili uweze kumsamehe mwenzako na kufanya msamaha wa kweli ni lazima atambue kosa. Hivyo basi, usifanye msamaha kama mkosaji hajatambua kosa lake. Mfano ‘mtu anakwambia ni samehe basi, kama nimekukosea’ sasa kama hujamkosea unaomba msamaha wa nini? Ndio maana tunasema ni lazima mkosa atambue kosa lake kabla hajafanya msamaha wa kweli.

Mfano mwingine mtoto anaangalia tv akaambiwa zima tv huu ni muda wa kusoma basi mtoto anaanza kulia, kujitupatupa chini, kujigaragaza na kubamiza milango na kuonekana kama vile amekosewa. Sasa mzazi mwingine badala ya kumuacha mtoto atambue kosa lake mzazi anamtetea na hatimaye mtoto anaona kama hana kosa. Kama mzazi usitishike mtoto akilia mwache alie na baadaye atatulia na kutambua kosa lake.

Hivyo kuna watu wengi wanafanya msamaha pasipo kuchunguza kiini cha kosa, kutotambua kosa. Katika kufanya msamaha pitia hizo hatua hapo juu. Unatakiwa kushinda ubaya kwa wema. Usilipe kisasi wewe samehe kutoka moyoni usipambane na mtu, samehe uwe na amani, furaha na afya njema. Kumbuka uponyaji wa kweli unaanzia moyoni.

Wasamehe watesi wako hata kwa machozi na achilia fundo lililo moyoni. Hata ukikumbuka ulipotoka na ulipo na unaona machozi yanatoka lia tu na uchungu utoke moyoni. Msamaha wa uongo unaongozwa na hisia na msamaha wa kweli unatoka moyoni na hauna masharti.

Post a Comment

Previous Post Next Post