SMS ZA MAHABA


Raha kwako naipata, hakika nimeridhika,
Kwako hakuna matata, moyo wangu umefika,
Usiku ninakuota, kwako naliwazika,
Siogopi kukupenda, hata watu wakisema.

Upendo uso kipimo, wewe nimekupatia,
Moyo unalo tuwamo, raha naipata pia,
Kwenye moyo wangu umo, raha yangu ya dunia,
Siogopi kukupenda, hata watu wakisema.

Wenye kusema waseme, waseme hadi wachoke,
Roho zao ziwaume, ziwaume wakereke,
Mioyoni ziwachome, wachomeke wakauke,
Siogopi kukupenda, hata watu wakisema.

Wenye wivu uwashike, uwashike uwagande,
Zaidi wahuzunike, wahuzunike wakonde,
Chakula kisiwashuke, wacha mie nikupende,
Siogopi kukupenda, hata watu wakisema.

Ni raha mwangu moyoni, wewe kuwa ndiwe wangu,
Nimezama furahani, rahani chini ya mbingu,
Sisi tumo mapenzini, tuache ya walimwengu,
Siogopi kukupenda, hata watu wakisema. 

Post a Comment

Previous Post Next Post